Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Ofisi ya mwanasheria mkuu wa serikali
AALCO WALAANI MAPIGANO BAINA YA ISRAEL NA PALESTINA
service image

   Nchi Wanachama wa  Taasisi ya Mashauriano ya Sheria za Asia na Afrika ( AALCO)   kwa kauli  moja  wamelaani  vikali  vurugu zinazoendelea kati ya  Palestina na Israel na kuzitaka nchi hizo mbili kutafuta suluhu kwa njia ya amani

 Kauli hiyo dhidi ya machafuko yanayoendelea baina ya  Israel na  Palestina ni Baadhi ya maazimio yaliyofikiwa   mwisho mwa Mkutano wa 61 AALCO uliokuwa ukifanyika katika Mji wa Bali nchini Indonesia.

 Wanachama wa AALCO ,   wameazimia  pamoja na mambo mengine,  kuendelea kushirikiana katika kuboresha kazi za Tume ya Sheria za Kimataifa inayosimamiwa na AALCO.

 Mkutano huo  ambao ulikuwa wa wiki moja,   pia umeazimia kuendelea kutoa ushirikiano   kwa  AALCO katika jitihada zake za kuwajengea uwezo wanasheria katika Sheria za Kimataifa hususani   Sheria za Bahari na Sheria za kimataifa za Uwekezaji na Biashara.

Ujumbe wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu  wa Serikali katika  Mkutano huo, uliongozwa na  Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Balozi Kennedy  Gaston.

Pamoja na  kuhudhuria na  kushiriki vikao mbalimbali vya Mkutano huo,  Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali pia   alipata fursa ya kubadilishana Mawazo  na Viongozi mbalimbali waliohudhuria  Mkutano  akiwamo  Waziri wa Sheria na Haki za Binadamu wa Indonesia  Bw. Yasonna H. Laoly.

Waziri  Laoly pia ni Rais  wa Taasisi  ya AALCO kwa mwaka 2023/2024.

 Katika  mazungumzo hayo Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali  amempongeza Waziri Laoly kwa  namna alivyoongoza mkutano huo kwa ufanisi na akamuahidi ushirikiano wakati wa kipindi chote cha uongozi wake kwenye Taasisi hiyo.

Naye Waziri Yasonna Laoly alimpongeza  Mhe. Balozi Gaston kwa  kuteuliwa kuwa Naibu Mwanasheria Mkuu wa  Serikali  huku akimtakia kila la kheri  katika utekelezaji wa majukumu  yake. 

Mwisho

22/10/2023

21 Oct, 2023
Maoni