Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Ofisi ya mwanasheria mkuu wa serikali
AG FELESHI AHAIDI KUSIMAMIA MAELEKEZO YA SERIKALI
service image

Na Mwandishi  Maalum

Kutoka  Viwanja vya  Chinangali

Dodoma

 Mwanasheria Mkuu wa Serikalil Mhe. Jaji Dkt. Eliezer Feleshi amemhakikishia  Mhe. Samia Suluhu  Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwamba,  ataendelea kusimamia kwa karibu maelekezo aliyotoa tarehe 29 Septemba 2022 ambayo yalitokana na  maelekezo ya awali ambayo yeye Mwanasheria Mkuu wa Serikali  aliyatoa kwa  Watendaji wa Serikali.

Maelekezo hayo  ni ya kuwataka  Watendaji Wakuu wa Serikali  pamoja na mambo mengine kutoa kipaumbele cha kumaliza migogoro kwa njia ya  usuluhishi. Aidha Rais  Samia Suluhu  Hassani aliwataka   septemba 29 2022 akizindua Chama cha  Mawakili wa Serikali  pamoja na mambo mengine  aliwataka Mawakili wa Serikali    kuhakikisha  wanakuwa makini  kusikiliza migogoro na kuhakikisha inatatuliwa  kabla ya kufikishwa mahakamani.

 Mhe. Feleshi   amesisitiza kuwa   Ofisi yake (OMMS) na Ofisi ya Wakili  Mkuu wa Serikali (OSG)  pia zitaendelea kutekeleza    maelekezo    ya kusimamia kwa  niaba ya serikali  matakwa ya kisheria ya kutatua migogoro kwa njia ya usuluhishi.

Mwanasheria  Mkuu Feleshi ametoa ahadi hiyo leo  Jumatano  wakati alipokuwa akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Shera Nchini ambapo  Mhe. Rais alikuwa mgeni rasmi.  Maadhimisho hayo yamefanyika katika  viwanja vya Chinangali  Jijini Dodoma na kuhudhuriwa na  viongozi wa mahakama,  serikali, bunge,  mawakili,  wanafunzi na  wananchi.

 Mwanasheria  Mkuu wa Serikali  aliyezungumza  katika hadhara hiyo  muda mfupi  mara baada ya  Rais wa Chama cha Mawakili wa Kujitegemea ( TLS) Profesa  Edward Hosea , amesema  , pamoja na kutekeleza  maelekezo aliyoyatoa  Mhe Rais pia ataendelea kusimamia maelekezo aliyoyatoa  kama  Mwanasheria Mkuu wa Serikali mnamo March  30,2022 kwa Watendaji Wakuu Serikalini la kuwataka pamoja na  mambo mengine kutoa kipaumbelea cha kumaliza migogoro kwa njia ya maridhiano.

Mhe. Feleshi amebainisha  pia kwamba,    maelekezo  yake hayo pia   aliyapeleka kwa  Mhe. Katibu Mkuu  Kiongozi  ambaye naye  aliwasisitiza watendaji  wa  serikali  kuwa  hatua ya uvunjaji wa mikataba iwe ni suluhisho la mwisho baada ya njia zote za majadiliano kushindikana na kwamba uvunjaji huo ufanyike kwa kibali cha Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Pamoja na kusisitiza kuwa atasimamia maelekezo  ya Mhe. Rais na yale ambayo  yeye aliyatoa kama Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Mhe. Jaji Dkt, Eliezer Feleshi akatumia  hadhara hiyo kuwakumbusha watendaji wa Serikali  kuzingatia maelekezo hayo muhimu

Ili kuiishi kwa vitendo  kauli mbiu ya siku ya sheria nchini kwa mwaka 2023. Mwanasheria Mkuu wa Serikali  ametoa rai  kwa waheshimiwa Majaji na Mahakimu kuwa tayari kuwasilisha Ofisini  kwake kupitia dawati linaloshughulika na utendaji kazi wa Mawakili wa Serikali kuhusu wakili yeyote wa Serikali ambaye kwa namna yoyote atathibitika kudhoofisha jitihada za Serikali na Mahakama  za kutumia njia za usuluhishi katika kutatua migogoro.

Katika  hatua nyingine Mwanasheria Mkuu wa Serikali  amesema  wakati umewadia wa kuboresha tena  Sheria ya Mwenendo wa Madai, Sura ya 33 ili  shauri la madai lipate sifa ya kusajiliwa  mahakamani  endapo kuna uthibitisho kwamba limepitia hatua zote za usuluhishi na ikashindikana.

Kwa upande wake    Rais Samia Suluhu  Hassan  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  ameagiza  Wizara ya Katiba na Sheria,   Wizara ya Fedha na Mwanasheria Mkuu wa Serikali  kushirikiana na  kuzifanyia marekebisho sheria zenye mizunguko mingi na hivyo kuchelewesha utoaji wa haki.

Naye Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Profesa Ibrahim Juma  amepongeza mapendekezo  yaliyotolewa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali  wa kuzifanyia mabadiliko baadhi ya sheria zenye milolongo mirefu na kwamba  marekebisho hayo yatasaia sana.

Vile vile  Jaji Mkuu  ametoa rai  pia kwa  Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuhakikisha kuwa suala la usuluhishi wa migogoro  nje  ya mahakama liwe la lazima na jambo hilo limo ndani ya uwezo wake.

 

Kauli  mbiu ya Siku ya  Sheria  nchini ilikuwa  umuhimu wa utatuzi wa Migogoro kwa njia ya usuluhishi katika kukuza  uchumi Endelevu:  Wajibu wa Mahakama na Wadau”.

Imeandaliwa na Kitengo cha Mawasiliano

01/02/2022

02 Feb, 2023
Maoni