Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Ofisi ya mwanasheria mkuu wa serikali
AG FELESHI AONGOZA KIKAO KUHUSU MASUALA YA UWEKEZAJI NCHINI
service image

Na Mwandishi Wetu

03/08/2022

Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Jaji Dkt. Eliezer Feleshi jana  Jumanne amekuwa na kikao na  Viongozi kutoka  Wizara na Taasisi  ambazo  kwa namna moja ama nyingine, zinahusika na  masuala ya uwekezaji.

Mhe. Mwanasheria Mkuu  aliitisha  kikao hicho  kufuatia  uwepo wa changamoto na malalamiko  kutoka kwa baadhi ya  watu wanaotaka kuwekeza nchini.

Baadhi ya  changamoto hizo au malalamiko hayo  ni  kuhusu utendaji wa Taasisi za Serikali, wimbi kubwa la  migogoro  ya  uwekezaji katika  mabaraza ya  usuluhishi ya Kimataifa pamoja na  kukosekana kwa utaratibu mzuri wa pamoja katika kushughulikia  changamoto hizo.

Kikao hicho cha siku moja  na ambacho pia kilihudhuriwa na   Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali Dkt. Evaristo  Longopa kililenga  kuzijadili changamoto  hizo pamoja na  namna bora ya  kuzishughulikia.

Wizara na Taasisi zilizohudhuria  kikao hicho  kilichofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali  Mtumba Dodoma ni  Ofisi ya Rais Ikulu, Wizara ya Fedha na Mipango, Ofisi ya Rais TAMISEMI, Wizara ya  Uwekezaji, Viwanda na Biashara, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Wizara ya Katiba na Sheria.

Taasisi  nyingine  zilizoshiriki kikao hicho ni  Kituo cha Uwekezaji  ( TIC) na  Mamlaka ya Maeneo  Maalum ya  Uzalishaji  kwa  Uwekezaji wa Mauzo ya Nje (EPZA) na   Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

 

 

 

03 Aug, 2022
Maoni