Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Ofisi ya mwanasheria mkuu wa serikali
AG FELESHI AWAPA SOMO MAWAKILI WA SERIKALI WAPYA
service image

Na Mwandishi Maalum

DODOMA

10/08/2022

Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Jaji Dk. Eliezer Feleshi  ameelezea nia na adhama yake ya  kurejesha heshima  ya  Mawakili wa Serikali.

Ameonyesha  nia hiyo leo ( Jumatano) wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na  Mawakili  wa Serikali  48 ambao wameajiriwa hivi karibuni.

Katika  mazungumzo hayo  na ambayo  pia yalihudhuriwa na  Mkurugenzi wa Mashtaka ( DPP) Bw. Sylvesta Mwakitalu,  Mwanasheria Mkuu wa Serikali  amesema  anatarajia kuirejesha heshima  kwa Mawakili wa Serikali  kama ilivyokuwa miaka  kadhaa ya nyuma,

“Tuliona  tukutane nanyi ili  tuweze kufahamiana, kuelezana  masuala ya awali  kabla  hamjaendea kwenye Vituo  vyenu vya kazi. Lakini  ninataka mtambue ukubwa wa dhamana na heshima tuliyowapa ya kuwa Mawakili  wa Serikali. Kubwa kwenu ni  kutambua  nyinyi sasa ni   Mawakili wa Serikali” Akasitiza Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Akawaeleza  Mawakili  hao  ambao  ajira yao  imezingatia uwiano wa  jinsia kuwa  “ Miaka kadhaa iliyopita,   tulikuwa    tunasema, sisi ni zaidi ya Bunge, ni zaidi ya Mahakama siyo kwa bahati mbaya ni kutokana na  majukumu yetu na mfumo   wa utekelezaji wa majukumu  yetu, ningependa kuirudisha heshima hiyo kuanzia kwenu  hasa  kutokana na  mchujo mkubwa  tulioufanya mpaka kuwapata”.

 Akizungumzia  namna  Mawakili hao  walivyopatikana. Mwanasheria Mkuu  wa Serikali  ameeleza kuwa  zaidi ya watu 1000  waliomba  nafasi ya kuajiriwa. Baada ya mchujo   mkali walipatikana watu   272 ambao nao walichujwa hadi kupatikana  Mawakili  hao  48.

Mwanasheria Mkuu  amewataka   Mawakili hao  ambao  kabla ya kuajiriwa Serikali walikuwa ni   mawakili wa kujitegemea , kuwa sasa wanatakiwa kujitofautia na Mawakili  wa kujitegemea.

 Amewatahadharisha Mawakili hao  kujiepusha na  vitendo vitakavyokwenda  kinyume na   maadili ya utumishi wa umma,  vikiwemo  vitendo ya  rushwa.

“Niwaombe sana mkazingatie maadili  ya utumishi wa umma.  Hivi  itakuwaje baada ya  muda nipate taarifa kuwa miongoni mwenu kuna waliochukua rushwa,  jiepusheni na vitendo kama hivyo mkatende haki,  nafahamu kuna vishawishi vingi, lakini ukikumbana na  hali kama hiyo sisi viongozi wenu milango ipo wazi njooni kwa ushauri”.

Pamoja na  kuzingatia maadili ya utumishi wa umma  na dhamana waliopewa, Mwanasheria Mkuu  wa Serikali  amesisitiza  pia  suala  na unadhifu kwa Mawakili wa Serikali  kuwa ni jambo ambalo ni lazima na si la hiari.

Akawataka  kujijengea utamaduni wa kujiendelea wakiwa kazini,  kuwa wabunifu na wanaopeda kujifunza  na kuonya  Wakili yeyote ambaye  atapuuzia suala la kujiendeleza na kujiongezea maarifa atakuwa ni aduni mkubwa.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Mashtaka Bw. Sylvester  Mwakilitalu    amewaeleza  Mawakili hao  kuwa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali,  Ofisi ya Taifa ya Mashtaka na  Ofisi ya Wakili  Mkuu wa Serikali ni   Ofisi kubwa, nyeti na  zenye majukumu makubwa kwa Taifa .

“Majukumu ambayo sasa mnakwenda kuyafanya ni majukumu nyeti na makubwa. Mtafanya maamuzi ya kushtaki au kutoshtaki. Maamuzi hayo ukiyakosea kuna haki ya mtu itapotea na  kuna muathirika  hata pata haki yake”. Akatahadharisha DPP.

“ Katika utekelezaji wa majukumu yenu,  mtatoa  ushauri, ushauri wako unaweza  kuliingiza taifa kwenye hasara na shida kubwa, kwa hiyo mnaweza kuona  ukubwa wa majukumu yenu, wengi hapa mmetoka kwenye kampuni binafsi za uwakili   tunatarajia mtafanya kazi zenu kwa weledi, kwa uaminifu na kwa kuzingatia miiko ya sheria,”

Aidha  amewataka mawakili hao kutambua kwamba sasa wao ni maafisa wa mahakama  kwa sababu hiyo wanatakiwa kuisaidia  mahakama katika kutenda haki kwa mujibu wa sheria na   kuachana na  ujanja janja.

Mawakili hao  pia  walikula kiapo  cha ahadi ya Uadililfu kwa  Utumishi wa Umma zoezi liloendeshwa na  Naibu Mkurugenzi wa Mashtaka Bw. Joseph Pande. Viongozi  wengine waliohudhuria mazungumzo hayo ni  pamoja na  Kaimu  Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali   Bw. Onorius Njole na WSakurugenzi wa Utawala  na Raslimali watu  kutoka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Ofisi ya Taifa ya Mashtaka.

 

10 Aug, 2022
Maoni