Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Ofisi ya mwanasheria mkuu wa serikali
DAG GASTON AHAIDI USHIRIKIANO NA FURAHA KWA WATUMISHI WA OMMS
service image

Na Mwandishi Maalumu

 

Naibu Mwanasheria  Mkuu wa Serikali  Balozi, Prof.  Kennedy Gaston   ameahidi kumsaidia Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe.  Jaji Dkt. Eliezer  Mbuki Feleshi  kwa kutekeleza majukumu yake kwa ueledi.

Ametoa  ahadi hiyo leo  Alhamisi  ( Septemba  14,2023)   wakati alipowasili  katika Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali  Mkoani Dar Es Salaam   muda  mfupi mara  baada ya kuapishwa  na Mhe. Samia Suluhu Hassan  Rais wa Jamhuri ya Muungano  ya Tanzania kuwa  Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali  katika  hafla iliyofanyika Ikulu ya Magogoni Jijini Dar es Salaam.

Alipowasili katika Ofisi ya  MMS Mkoani Dar  Es Salaam alipokelewa na  Mwanasheria Mkuu wa Serikali Dkt.  Feleshi, Mwandishi Mkuu wa Sheria  Onerius Njole,  Mkurugenzi wa Utawala na  Raslimali Watu  Silas Marwa , Wakili wa Serikali  Mkuu Mwema Pumzi,  Mawakili wa Serikali na  watumishi  wanaohudumu katika Ofisi ya Mkoa wa  Dar es Salaam

Pamoja na kutoa  ahadi hiyo ya kumsaidia  Mwanasheria Mkuu wa Serikali,  Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali  Balozi Prof, Gaston pia ameahidi  ushirikiano, mshikamano  na  kuendeleza yale yote ambayo  yamekuwa yakifanyika ikiwa ni Pamoja na kuendelea  kuwajengea uwezo watumishi na  kuwafanya watumishi wote wa OMMS kuwa watu wenye furaha.

 “Kwanza  nishukuru sana kwa mapokezi  mazuri, niseme ,nimeheshimiwa sana kuwa  mwanachama  ya timu ya Ofisi ya Mwanasheria  Mkuu wa Serikali, nikiwa  mwanachama mpya ninaahidi kuwa mwanachama hai nitakayeendeleza  kulizungusha gurudumu  katika  Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali  ili   Pamoja na  mambo mengine  kazi iendelee” akasema Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali  na kuongeza

“Wataalamu  wana msemo  wao kwamba,  chumba kisichojaa ni chumba ambacho  kinahitaji maboresho hivyo nina amini  kuwa  bado ninayo nafasi kubwa ya  kuchangia  maboresho ya  Ofisi ya Mwanasheria Mkuu  wa Serikali”.

Akizungumza  Zaidi  katika  hafla hiyo ya kumkaribisha, Balozi Gaston alimuahidi Mwanasheria Mkuu wa Serikali  kwa kusema, yeye kama Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali atakuwa  wa kwanza kati ya walio sawa ( the first among the equals) na kwamba itakuwa timu itakayofanya kazi na kukaa Pamoja.

 Kwa upande wake Mwanasheria Mkuu wa Serikali  Mhe. Jaji Dkt. Eliezer Feleshi  akimkaribisha Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali  Pamoja na  kumhakikishia ushirikiano wa hali ya juu alisisitiza kwa kusema yeye ( Mwanasheria Mkuu ) anapenda Ofisi yake iwe na watu wenye furaha lakini  pia wachakapakazi.

 

“ Kanuni yangu ni  1+5 yaani  kila Wakili wa Serikali Mwandamizi lazima awe na  watu watano nyuma yake kwaajili ya  kujenga timu  imara, hii ndiyo kanuni yangu” akasisitiza  Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

 Akizungumza  kwa niaba ya  Watumishi wa Ofisi ya MMS Mkoa wa Dar Es Salaam, Wakili  wa Serikali  Mkuu Mwema Pumzi alimuahidi  ushirikiano wa hali ya juu  Naibu Mwanasheria  Mkuu wa Serikali  katika utekelezaji wa Majukumu yake.

Mwisho

 

 

 

 

 

 

 

15 Sep, 2023
Maoni