Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Ofisi ya mwanasheria mkuu wa serikali
JICA YAONYESHA NIA YA KUSHIRIKIANA NA OFISI YA MWANASHERIA MKUU
service image

Na Mwandishi  Maalumu

Shirika la  Maendeleo  la Kimataifa la Japani ( JICA)  limeelezea nia yake  ya  kutaka  kushirikiana na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali katika maeneo mbalimbali.

Nia hiyo ya JICA, imeelezwa  leo ( Jumatatu )na Bw.  Asano Siezaburo mwakilishi wa JICA Ofisi ya Tanzania, wakati  walipokutana na  kufanya  mazungumzo na  Kaimu Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali  Bw. Onorius Njole.Mazungumzo yaliyofanyika katika Ofisi ya  Mwanasheria Mkuu wa Serikali  Mtumba, Jijini Dodoma.

“ Tumekuja    tujadiliane  na kuona   ni maeneo gani  Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali inaweza kunufaika na misaada inayotolewa na  JICA, hii ni kwa sababu  tunataka kuwa na  ushirikiano na Ofisi hii”. Akabainisha  Bw. Seizaburo aliyekuwa ameambatana na  Bi. Yukiko  Karanuki katika mazungumzo hayo.

Moja ya  eneo ambalo  JICA imeonyesha nia  ya  kutaka  kusaidia    ni katika eneo  la kujenga uwezo ( Capacity Building)  kwa Mawakili wa Serikali.

Kwa kuanzia JICA itatoa fursa  kwa  Mawakili  watatu (3 ) kwenda kujengewa uwezo kwa kuwapatia mafunzo katika eneo la Sheria za Biashara.

Ujumbe huo wa JICA  umeitaka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali  kuainisha maeneo mengine ya ushirikiano na kisha  kuwasilisha JICA kwa  majadiliano zaidi.

Kwa upande wake Kaimu Naibu Mwanasheria  Mkuu wa Serikali Bw. Njole  ameishukuru   JICA kwa   kuona umuhimu  wa  kutaka  kuwa na  ushirikiano  na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Akasema ,  huduma za Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ni  mtambuka  zinazogusa kila  sekta ya nchi hii na kwa sababu hiyo  nia hiyo ya JICA ya kutaka kuwa na  mahusianao na OMMS ni muhimu sana.

“Karibu  katika  kila misaada ambayo JICA  inatoa   hapa Nchini iwe  TANESCO  kama ulivyosema, au katika Sekta  yoyote ile, kuna mkono wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, na hili halikwepeki kwa hiyo kila mnapotoa ushirikiano  katika  sekta  fulani  basi muikumbuke Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.   Mmefanya  vema kuona   umuhimu wa Taasisi hizi mbili kuwa na  majadiliano ya kuona namna gani tunaweza  kushirikiana”. Amesisitiza  Bw. Onorius Njole ambeye pia ni Mwandishi Mkuu wa Sheria.

Aidha,  Kaimu Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali  ameishukuru JICA pia   kwa kutoa  fursa  ya kuwajengea uwezo Mawakili wa Serikali  katika  eneo la  Sheria za Biashara na kwamba  mwanzo huo ni  mzuri.

Akaahidi  kwamba,  Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali  itaangalia  maeneo mengine ya ushirikinao

Katika  mazungumo hayo, Kaimu Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali aliambatana na Bi.Slyvia Matiku,  Mkurugenzi  Msaidizi Divisheni ya  Uratibu na Huduma za Kisheria na  Bw. Sunday Hyera Mkurugenzi Msaidizi  Divisheni ya Mikataba .

11/7/2022

 

11 Jul, 2022
Maoni