Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Ofisi ya mwanasheria mkuu wa serikali
KAMATI YA BUNGE YAPONGEZA MRADI WA KITUO JUMUISHI CHA TAASISI ZA KISHERIA ZA SERIKALI
service image

Na Mwandishi  Wetu

Busweru - Mwanza

Kamati  ya kudumu ya   Bunge ya   Utawala, Katiba na Sheria imeupongeza   mradi  wa Ujenzi wa Kituo   Jumuishi  cha Taasisi za  Kisheria za Serikali na kuuelezea kuwa ni mradi wa mfano wa kuigwa.

 Wametoa pongezi hizo leo Alhamisi wakati walipoutembelea mradi huo unaojengwa na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali  katika  Kata ya Busweru Wilaya ya Ilemela Mkoani  Mwanza.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti mara baada ya kupata maelezo ya mradi huo  na kisha kuutembelea, Wabunge hao wametaka  mradi huo ukamilike kwa wakati  kama ilivyo kwenye mpango kazi.

Zaidi ya wabunge tisa (9) wa kamati hiyo waliuliza maswali mbalimbali kwa  Mkandarasi (SUMA-JKT) na Mshauri  elekezi (TBA) mengi ya maswali hayo yaliyoambatana na pongezi na yalitaka   ufafanuzi kuhusu  mradi.

Akizungumza mara baada ya  wabunge hao  tisa kupata fursa ya  kuuliza maswali Makamu  Mwenyekiti wa Kamati hiyo  Mhe. Florent Laurenti Kyombo (Mb) alimtaka Waziri wa Katiba na Sheria  kuyafanyia kazi baadhi ya masuala yaliyoibuliwa na  wabunge hao.

“Mhe. Waziri (Ndumbaro) sisi Kamati ya Bunge ya Utawala,  Katiba na Sheria  tumeridhishwa na  kazi inayoendelea hapa, huu ni mradi mzuri na  wa viwango, tunakupongeza  sana  sasa ukayafanyie kazi  yale  masuala madogomadogo  tuliyoyaeleza hapa” akasema Makamu  Mwenyekiti wa Kamati.

Akaongeza kwa kusema  miradi kama hii inayosogeza huduma za kisheria karibu na wananchi na ambayo ndiyo dhamira   ya Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha  wananchi wanapata huduma za kisheria  bila usumbufu wowote.

“Miradi  kama hii ambayo ni ya mfano  inatupatia sisi  wajumbe nguvu ya Kwenda kuizungumzia kwenye kamati  zetu na kuziombea fedha ili  iweze kuenea nchi nzima”. Akaseme Mhe Kyombo.

Akijibu hoja za wabunge hao  ikiwamo ya mapendekezo ya  mkandarasi kuongezewa muda kwa kile walichosema mradi upo  nyuma kwa miezi miwili  Waziri alikuwa na haya ya kusema.

“ Waheshimiwa wabunge  niwashukuru sana kwa kuutembelea mradi huu na kwa ushauri mlioutoa kuhusu  suala la kumuongezea muda mkandarasi nieleza wazi  kabisa,  Serikali haikusudii na wala haitamuongezea   muda, mkandarasi afanya analoweza kufanya aukamilishe mradi huu  kulingana na makubalianao  ambapo ni mwezi Octoba  Mwaka huu.” Akasisitiza Waziri na kuongeza.

Serikali  itaendelea kutoa ushirikiano  kwa mkandarasi na  mshauri mwelekezi wakati wowote watakapokuwa wana tatizo na ikibidi  hata kubadili mfumo wa malipo.

Akatahadharia  kwa kusema endepo  mkandarasi hata kamilisha mradi huo kwa wakati basi itampasa kuilipa serikali   kama  taratibu zinavyotaka.

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya  Kudumu  ya Utawala,  Katiba na Sheria  ilikuwa mkoani  Mwanza ambapo pamoja na  kuutembelea mradi wa Ofisi ya Mwanasheria wa Serikali  pia wametembelea  Jengo  Jumuishi la Utoaji  haki la Mahakama ya Tanzania.

Kabla kutembelea miradi hiyo walimtembelea Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe Kigoma  Malima  ambapo walipokea taarifa ya mkoa.

Kamati hiyo ya Bunge  kabla ya kufika Mkaoni Mwanza,   walikuwa  Mkoa wa  Shinyanga na Tabora.

Mwisho

Imeandaliwa na  Kitengo cha Mawasiliano

 

16 Mar, 2023
Maoni