Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Ofisi ya mwanasheria mkuu wa serikali
SAMIA ATIMIZA AHADI YAKE KWA MAWAKILI WA SERIKALI
service image

Na Mwandishi Maalum

 

Dodoma.  Rais Samia Suluhu Hassan ametoa  komputa mpakato  150  kwaajili ya  mawakili wa  serikali  ikiwa ni ahadi yake  aliyoitoa wakati wa Mkutano Mkuu wa Mawakili wa Serikali uliofanyika Mwezi Septemba 2022.

  Vifaa hivyo vya  Tehama,  vimekabidhiwa jana jumatano  kwa  Mwanasheria Mkuu wa Serikali  Mhe. Jaji  Dkt. Eliezer  Feleshi na Katibu Mkuu Kiongozi  Mhe Dkt Moses Mpogole Kusiluka  aliyekabidhi kwa niaba ya Mhe. Rais  katika  hafla fupi iliyofanyika  Ikulu na kushuhudiwa  na Mkurugenzi wa  Mashtaka Bw. Sylvester  Mwakitalu na  Wakili Mkuu wa Serikali  Dkt. Boniphace  Luhende.

Akizungumza katika hafla ya hiyo ya makabidhiano,   Katibu Mkuu Kiongozi amesema,  ni matumaini ya  Mhe. Rais kuwa, vifaa hivyo vya tehama  vitaboresha  na kuongeza ufanisi  wa mawakili wa serikali katika utekelezaji wa  majukumu yao.

“Tumekutana katika hafla hii fupi lakini muhimu sana.  Mhe Rais alitoa maelekezo tukutane ili nikukabidhi vifaa hivi vya Tehama  ambayo Mhe Rais aliridhia  wakati wa Mkutano Mkuu wa Mawakili wa Serikali  uliofanyika mwezi septemba 2022 hapa Dodoma”. Akaeleza  Katibu Mkuu  Kiongozi

Na kuongeza “ Ni  matarajio ya  Mhe. Rais kuwa vitendea kazi hivi   vitatumika kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu  yao mawakili wa serikali  na hasa kwa kuzingatia umuhimu wa  matumizi ya tehama katika tasnia ya  sheria”.

 Katibu  Mkuu kiongozi  Kusiluka akaeleza zaidi kwa kusema “ Sote tunafahamu Mhe. Rais  ametoa kipaumbele  katika kuboresha mifumo ya haki jinai na haki  kwa ujumla, hivyo  basi   juhudi za Rais na serikali  kupitia msaada huu  ni kuona  ufanisi  wa mawakili  wa serikali  nao unaongezeka”.

Vile vile  Mhe. Kusiluka   amesisitiza kuwa  Serikali  itaendelea kuwasaidia  Mawakili wa Serikali  kadri  itakavyowezekana  hasa katika  kipindi hiki ambacho  Serikali  imejikita katika utekelezaji wa miradi ya kimkakati, miradi ambayo inahitaji wataalamu wabobevu katika kila eneo  wakiwamo  Mawakili wa Serikali.

“ Serikali inathamini  mchango  wa mawakili wa serikali, ni  matumaini ya Rais na ya kwangu kwamba, nyinyi viongozi wa Taasisi mtaendelea  kusaidia na kuhamasisha wataalamu wenu  kuisaidia  serikali katika utekelezaji wa miradi hii ya kimkakati” akasisitiza  Katibu Mkuu Kiongozi.

Kwa upande wake akizungumza  baaada ya kukabidhiwa vifaa hivyo vya Tehama,  Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Jaji Dkt. Eliezer   Feleshi  amesema    Komputa  mpakato hizo  zitaleta  heshima kubwa kwa mawakili wa serikali.

“Kwa niaba ya  Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali,  Ofisi ya  Taifa ya  Mashtaka na Ofisi ya Wakili  Mkuu wa Serikali,  nitoe shukrani zangu za dhati kabisa kwa Mhe. Rais  kwa kuridhia  na kutupatia  vifaa hivi vya tehama ametuangalia  kwa jicho la umama na kwa kweli ni  upendo wake wa dhati” akasema Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Akasema ,  wakati wa mkutano Mkuu wa Mawakili wa Serikali  uliofanyika   Septemba 29 mwaka jana , Mkutano ambao  Mhe.  Rais  alikuwa  mgeni rasmi na pia  akazindua  Chama cha Mawakili wa Serikali  alibainisha  changamoto mbalimbali zikiwamo za  uhaba wa vitenda kazi  kwa maana  ya Vifaa  vya  Tehama kwa  mawakili wa Serikali  

“Katika  Mkutano ule  tulielezea changamoto mbalimbali  zikiwamo za miundombinu, upungufu wa  watumishi ,lakini tukaelezea hili la  vitendea kazi kwa maana ya  vifaa vya tehema  ili kwenda sambamba na  maboresho yanayoendelea katika Tasnia ya Sheria”.  Akasema Mwanasheria Mkuu

“Hata katika  majadiliano ya  migogoro baina ya Serikali na wadau wetu vikao vingi vinafanyika kwa njia ya  Tehema jambo ambalo  mawakili wetu wapo  nyuma kutokana nakutokuwa na  na  vitenda kazi vya kisasa. Vifaa hivi vitaleta heshima  kubwa kwa mawakili wetu wa Serikali wanapokuwa katika utekelezaji wa majukumu yao” akasisitiza  Mhe. Feleshi.

Aidha Mhe  Feleshi  akasema, vifaa hivyo vya Tehama si kwamba  vinahitajika kwa Mawakili wa Serikali peke yao bali hata  kwa   Divisheni na Vitengo  wezeshi   akitolewa  mfano wa   Kurugenzi  ya Utawala na Raslimali Watu ,   Kurugenzi ya Mipango na Masijala

“ Mhe Katibu Mkuu  Kiongozi,  tunafahamu mchakato huu umegharimu fedha na muda wa Mhe Rais na Serikali, sisi sote hapa ni wateule wa  Rais na ukisha kuwa mteule wa  Rais huna mambo yako, tunafuatilia na kusikiliza shughuli za Mhe Rais niahidi kwamba tutatumia vifaa hivi  ili kwa pamoja na  Serikali  tuweze kuleta nafuu kwa watanzania” Amesisitza  Mhe. Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Mwisho

Imeandaliwa na Kitengo  cha Mawasiliano

22/03/2023

 

 

23 Mar, 2023
Maoni