Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Ofisi ya mwanasheria mkuu wa serikali
TUME YA RAIS YA KUBORESHA HAKI JINAI YAKUTANA NA WADAU MKOANI MWANZA
service image

Na Mwandishi  wetu

Wajumbe wa  Tume ya  Rais ya  kuangalia namna ya  kuboresha Taasisi za Haki jinai  wanaendelea na zoezi la kutembelea Taasisi  mbalimbali  pamoja na kukusanya maoni kutoka kwa viongozi wa Taasisi hizo na Makundi mbalimbali ya jamii.

Katika  kutekeleza  majukumu  hayo,  wajumbe hao  wamegawanyika katika  makundi tofauti.

Kuanzia siku ya    jumatatu  Marchi 6 ,2023) Mwenyekiti wa  Tume hiyo  Mhe. Jaji Mkuu  Mstaafu Mohammed   Othman  Chande  akiwa amefuatana  na baadhi  ya  wajumbe wa Tume   Mhe. Jaji Dkt .Eliezer  Feleshi   Mwanasheria Mkuu wa Serikali  na  Mkuu wa Jeshi la Polisi Mstaafu  Bw. Said Mwema  wapo  Mkoani Mwanza.

Wakiwa  Mkoani  humo  Wajumbe hao  pamoja na  kukutana na kufanya mazungumzo  na mwenyeji wao Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhe.  Adam Malima  wamepata  fursa ya  kutembelea  Taasisi  mbalimbali  za Haki  jinai  zikiwamo  vituo  vya Polisi    kikiwamo Kituo Kikuu cha Polisi Mwanza na  Gereza    Kuu la Butimba.

Wakiwa katika  Taasisi hizo,  Wajumbe hao  walipata taarifa kutoka kwa  viongozi wanaosimamia taasisi hizo ( Magereza na Polisi)  na  pia  waliweza  kuzungumza na  wafungwa.

Pia timu hiyo  ilipata fursa ya   kuwa  na kikao na  wakuu wa Taasisi za Haki jinai mkoani  Mwanza,   wakiwamo  Polisi , Magereza,  Takukuru,  Ofisi ya Taifa ya  Mashtaka ,  Uhamiaji, na Taasisi inayohusika na  Madawa ya  kulevya.

Aidha wajume wa Tume hiyo  pia walipata fursa ya kuwa na mikutano ya hadhara ambapo  pamoja na kuelezea     majukumu  ya   Tume hiyo. Mwanasheria Mkuu wa Serikali  alielezea kwa kina   na kutoa  elimu kwa wananchi  kuhusu   suala  zima  na maana ya Haki Jinai na mnyororo mzima wa haki  jinai.

Baada ya  Maelezo hayo ya kina Mwanasheria Mkuu wa Serikali   katika mkutano wake na  wananchi katika wilaya  ya  Misungwi alitoa  nafasi kwa wananchi  kuelezea kero zao  na hata kuuliza maswali   katika eneo hilo la uboreshaji wa haki jinai nchini

Itakumbukwa  kwamba Mwezi jaruani Mwaka huu,  Mhe.  Samia  Suluhu Hassan   Rais wa Jamhuri ya Muungano wa  Tanzania, aliunda  Tume ya Rais ya kuangalia namna ya kuboresha Taasisi za haki  Jinai  nchini  na akaipa Tume   kukamilisha kazi  ifikapo  mwezi April mwaka huu.

Tume hiyo inaongozwa na  Mhe. Mohammed Othman Chande  ambaye ni mwenyekiti,  Balozi Omben Sefue  Makamu Mwenyekiti na  wajumbe wakiwa ni Mhe.  Jaji  Dkt. Eliezer  Mbuki Feleshi, Mwanasheria Mkuu wa Serikali,  Profesa Edward Hosea, Said Ally Mwema,  Balozi Ernest Magu, Dkt. Laurean Ndumbaro na Bw. Omary Issa.

Imeandaliwa na Kitengo cha Mawasiliano

7/3/2023

07 Mar, 2023
Maoni